
Dar es Salaam. Uko usemi maarufu
usemao: ‘ Hujafa hujaumbika’. Kwa hakika mateso yatokanayo na matatizo
ya afya ni sehemu ya maisha ya mwanadamu. Kwa kuwa binadamu hatujui ghaibu, yaani mambo
yaliyo nje ya uwezo wa milango yetu ya fahamu, ni vigumu kutabiri hali
ya maendeleo ya afya zetu.
Kimsingi, hakuna ajuaye kesho kwani hiyo ni siri ya muumba wa mbingu na ardhi. Dunia ni sawa na kitendawili.
Hadithi ya kijana Waziri Shaban inatia simanzi
unapoisikia. Ana matatizo makubwa ya kiafya anayohitaji msaada kutoka
kwa wasamaria wema.
Maisha tofauti
Shaban (28) mkazi wa Gongolamboto, mkoani Dar es
Salaam, anaishi maisha tofauti na ya walio wengi duniani. Yeye anapumua
kwa kutumia mdomo badala ya pua kama ilivyo ada kwa wanadamu.
Hatua hiyo inatokana na ugonjwa wa nyama za pua
anaosema umekuwa ukimtesa kiasi cha kujitokeza hadharani akiomba msaada
kwa jamii ili hatimaye aweze kupata tiba na kuondoka na madhila hayo.
Historia ya ugonjwa huo anasema ilianza Februari
2009, baada ya kuugua mafua makali na koo kuwasha. Alitumia dawa za
kawaida bila ya mafanikio.
“Mimi nilijua ni mafua ya kawaida tu lakini kumbe
sio, kwani kila siku zilivyozidi kwenda nilianza kuona pua ikivimba
kwa ndani, jambo ambalo lilinishtua sana,” anasimulia mwanzo wa maradhi
yake yanayomtesa hadi leo.
Mwaka 2010 baada ya uvimbe kujitokeza nje ya pua,
alilazimika kwenda Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa matibabu zaidi.
Kinyume na matarajio yake, hakupata huduma yoyote mbali ya kuelezwa awe
anaripoti hapo kila baada ya miezi mitatu.
Tangu mwaka huo mpaka sasa, Shaban amekuwa
akiripoti hospitalini kama anavyoeleza: “Sikukata tamaa walivyokuwa
wakiniambia kurudi kila miezi hiyo bila ya kupewa dawa ya aina yoyote,
hadi waliponiambia kuwa nitoe Sh850,000 ili nifanyiwe upasuaji.”
Ugumu anaoupata
Familia yake
Ugumu anaoupata
Akizungumza kwa sauti ya mbali na taratibu, huku
akitumia mdomo kupumua, anasema maradhi yake yanamweka katika wakati
mgumu, kwani anashindwa hata kufanya shughuli za kumpatia riziki.
“Kama unavyojua ndugu yangu, mdomo unafanya kazi
mbili; kuongea na kupumua, hivyo siwezi hata kuongea sana kutokana na
hali yangu. Nimeambiwa naweza kupona kama nitafanyiwa upasuaji,’’
anasema na kuongeza:
“ Sina ndugu wa kunisadia kwani nimezunguka sehemu
mbalimbali kutafuta fedha lakini nimekosa. Najua Watanzania wenzangu
wanaweza kunisaidia na kurejea katika hali yangu ya kawaida.”
Familia yake
Shaban ni baba wa mtoto mmoja. Alioa mwaka 2009
kabla ya kupatwa na maradhi hayo. Alipokuwa mzima alitimiza wajibu wote
wa kuhudumia familia akiwa baba na nguzo ya familia. Hivi sasa amegeuka
ombaomba, anayezunguka kwa watu wamsitiri maishani.
Anamshukuru mkewe kwa kuendelea kumvumilia hadi
leo…“Unajua ukipata matatizo utashangaa kuona mwanamke anakukimbia au
anakufanyia unyanyasaji, lakini mke wangu anaendelea kunitia moyo na
kuzunguka huku na huko kutafuta fedha.”
Naye mkewe anayeitwa Anna John, anasema hawezi
kumkimbia mumewe , kwa kuwa maradhi yake ni sehemu ya majaribu ya maisha
yanayoweza kumkumba mtu yeyote.
“Sitomwacha mume wangu nitahangaika naye hadi
nihakikishe anapona. Ingawa sina kazi nitajitahidi kumtia moyo ili
afarijike,’’anaeleza.
Anaamini kuwa kama maradhi hayo yamempata mume
wake, yangeweza pia kumpata yeye. Ni kwa sababu hiyo haoni sababu ya
kumtekekeza mzazi mwenzake.
Kwa sasa Ana amekuwa nguzo ya famiia. Anahangaika
huku na huko kutafuta chochote kwa ajili ya kuihudumia famila yake ya
watu watatu.
SOURCE:MWANANCHI.
SOURCE:MWANANCHI.
No comments:
Post a Comment