Tuesday, 26 November 2013

Wananchi ‘wawashtaki’ viongozi kwa mbunge

Wasema hawachukui hatua za kushughulikia kero zinazowakabili kwa muda mrefu
Wananchi  wa Mtaa wa Mwanzomgumu katika Kata ya Bigwa,  Manispaa ya Morogoro, wamewashtaki kwa mbunge wa jimbo hilo, Abdullaziz Abood, viongozi wa serikali ya mtaa huo, kwa kile walichokielezea kuwa ni kushindwa kuwatumikia.
Wananchi hao walisema tatizo hilo pia liko katika Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro, ambayo haifanyi jitihada za kutosha, ili kuwaondolea kero mbalimbali zikiwemo kukosa baadhi ya huduma muhimu.
Abood alipita katika mtaa huo akiwa katika ziara yake ya kusikiliza kero za wananchi wa Kata za Bigwa, Mindu na Mkundi ambapo pia alikabidhi  vifaa mbalimbali.
 Msaada wa vifaa hivyo ambao ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi zake za wakati wa kampeni  za uchaguzi wa mwaka 2010, ni pamoja na  vyerehani, mabomba ya kusambazia maji, mawe, kokoto, mifuko ya saruji, mchanga na hundi za fedha.
Katika hali ambayo haikutarajiwa, wananchi wa Mtaa Mwanzomgumu, walisimamisha msafara wa mbunge Abood na  kumlalamikia kitendo cha viongozi wao kutowajali kwa maana ya kushughulikia kero zao.
Wananchi hao walisema eneo lao linakabiliwa na matatizo mengi, lakini viongozi wao hawafanyi jitihada za kupunguza kama si kumaliza kabisa matatizo hayo.
Walisema matatizo hayo ni pamoja na ubovu wa barabara, kutozwa Sh100 kwa kila ndoo ya maji, ili kuchangia huduma hiyo na kukosekana kwa kituo cha polisi.
Baada ya malalamiko hayo, Abood aliwaita viongozi wa eneo hilo ili wajadiliane naye kuhusu namna ya kutatua matatizo hayo, lakini waligoma.
Badala yake, walimtaka aende walikokuwa, lakini naye alikataa kwa sababu ratiba ya ziara yake ilimbana.

SOURCE: MWANANCHI.

No comments:

Post a Comment