MBUNGE wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe (CHADEMA), amesema
mikopo inayotolewa kwa wanafunzi wa elimu ya juu itazamwe upya akisema
kuwa lengo lake ni kuhakikisha watoto wanaotoka katika familia masikini
wananufaika nayo.
Zitto ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu wa CHADEMA, alitoa kauli hiyo
juzi mkoani Tabora wakati akihutubia mikutano mbalimbali ya kuimarisha
chama katika ziara yake inayoendelea kwenye Kanda ya Magharibi.
Alisema kuwa serikali imekuwa ikitoa mikopo hiyo kwa madaraja ya
ufaulu pasipo kuangalia mazingira ya upatikanaji wa madaraja hayo.
Kwa mujibu wa Zitto ni ngumu kwa watoto wengi wanaotoka katika
familia za kimasikini ambao kuanzia shule ya msingi wanasoma katika
shule zisizo na walimu wa kutosha, vitabu vya kiada na maabara,
wakaweza kupata daraja la kwanza na la pili yatakayowawezesha kupata
mkopo wa kujiunga na elimu ya juu.
“Nimepigiwa simu na kijana toka Nanyumbu, Mtwara ananieleza kuwa huu
ni mwaka wa pili anashindwa kuendelea na elimu ya juu licha ya kupata
nafasi, huku wazazi wake wakiwa hawana fedha na serikali haimpi mkopo
kwa sababu ya daraja lake la ufaulu,” alisema.
Alisisitiza kuwa wakati hali ikiwa hivyo kwa watoto wanaotoka katika
familia za kimasikini, watoto wa matajiri mikopo hiyo imekuwa halali
yao kwa kuwa kuanzia shule ya msingi wanakuwa wameshajengewa mazingira
ya kuipata.
Katika hali ya kusikitisha, Zitto alisema anashangazwa na hekima
aliyonayo Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philip Mulugo
aliyewataka wanafunzi walioshindwa kuendelea na elimu ya juu kwa kukosa
mikopo wakauze ng’ombe, mbuzi na kuku kwa ajili ya kuendelea na masomo.
“Hii ni kebehi na ulevi wa madaraka kwa Watanzania, serikali
inakusanya kodi inasemaje haina fedha ya kuwasomesha vijana wake? Mbona
posho za kutulipa sisi pamoja na safari za rais hazikosekani?” alihoji
Zitto.
Alisema ni wakati muafaka kwa mikopo inayotolewa kwa wanafunzi wa
elimu ya juu ikawa ni kwa gharama za kuishi na zile za masomo, kwamba
wanafunzi wasidaiwe bali wasome bure.
Source: Tanzania Daima.
|
No comments:
Post a Comment